1. Bismillahi ‘Aliyyun, Ya Ilahi Ya Rahimu
    Bismillahi Qawiyyun, nguvu ni Zako Qayyumu
    Bismillahi Ghafurun, toba ni Kwako Hakimu
    Heko kumi la rehema, Allah katujaalia.
  1. Bismillahi Basirun, unatuona wajao
    Bismillahi Samiun, tusikize viumbeo
    Bismillahi Munirun, nawirisha wakuchao
    Heko kumi la rehema, Allah katujaalia
  1. Rehema Zako Rabana, zeleya kila mahala
    Rehema za Subhana, zenda kwa hata kabwela
    Rehema za Maulana, kwa ‘asi na mcha Mola
    Heko kumi la rehema, Allah katujaalia.
  1. Awali ya Ramadhani, kumi limejaa heba
    Kwa kusoma Qur’ani, na kukithirisha toba
    Wokovu kwa waumini, Rabbi utupe haiba
    Heko kumi la rehema, Allah katujaalia.
  1. Tufunge tukihimidi, rehema zako Rabbana
    Tufunge tukikunadi, turehemu Ewe Bwana
    Tufunge tukiburudi, Amina Rabbi Amina
    Heko kumi la rehema, Allah katujaalia.
  1. Tukitaja jina Lako, tuburudike nafusi
    Tukiona waja Wako, tukukumbuke Mkwasi
    Tukiwa na Peke Yako, tujiepushe kuasi
    Heko kumi la rehema, Allah katujaalia.
  1. Tukwogope hadharani, na zaidi faraghani
    Kubali wetu ugeni, Ilahi Ya Rahmani
    Bila ya Kwako Manani, twende kwa mwengine nani?
    Heko kumi la rehema, Allah katujaalia.
  1. Takabali zetu dua, saumu na sala pia
    Waja tumejaa doa, pumzi zinafifia
    Hatutendi kwa kujua, Ya Rabbi twakulilia
    Heko kumi la rehema, Allah katujaalia.

Na Ahmed Rashid

(Visited 58 times, 1 visits today)

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

error: Content is protected !!