1. Allah jina takatifu, naanza ya Rahmani
    Kwa jina Lako Latwifu, baraka za Ramadhani
    Samehe hai na wafu, sote tuwe neemani
    Rabi turuzuku toba, ni kumi la ghufurani.

***

  1. Turudi Kwake Raufu, Yaayyuha waumini
    Tusijifanye vipofu, kuasi wetu Manani
    Tujipange safusafu, kwa toba misikitini
    Rabbi turuzuku toba, ni kumi la ghufurani.

***

  1. Allah Rabbi utuafu, tumezama madhambini
    Mja kiumbe dhaifu, hajali jema ni nini
    Hutesa hata siafu, amshinda hayawani
    Rabbi turuzuku toba, ni kumi la ghufurani.

***

  1. Nyoyo zetu zi jafafu, ni kavu hatubaini
    Rutubaye ni hafifu, tarutubishwa na nini
    Kama si zako Arifu, kwa wajao samahani
    Rabi turuzuku toba, ni kumi la ghufurani.

***

  1. Tutende uadilifu, amri ya yetu dini
    Tusione takilifu, kurejea kwa Rabbani
    Nyoyo ziingie khofu, tujue tu masikini
    Rabi turuzuku toba, ni kumi la ghufurani.

***

  1. Mola wetu ni Latifu, twaasi tu madhambini
    Atusamehe Raufu, huruma nyingi pomoni
    Kumi hili takatifu, fursa tusitupeni
    Rabi turuzuku toba, ni kumi la ghufurani.

***

  1. Leo hai kesho mfu, zitajapita awani
    Bila ya Mola kukhofu, hakuna cha nusurani
    Toba kitu maalufu, tutubu dhambi jamani
    Rabi turuzuku toba, ni kumi la ghufurani.

Na Ahmed Rashid.

(Visited 12 times, 1 visits today)

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

error: Content is protected !!