Ajuza wa miaka 102 nchini Nigeria ametangaza nia yake ya kugombea urais wa nchi hiyo ya magharibi mwa Afrika unaotarajiwa kufanyika mwakani 2023.

Kwa mujibu wa tovuti ya “Naija News,” Bikizee Nonye Josephine Ezeanyaeche ametangaza nia yake hiyo mbele ya vyombo vya habari jijini Abuja. Ametoa tangazo hilo kwenye ofisi za Mamlaka ya Televisheni ya Nigeria NTA.

Bi Ezeanyaeche ambaye ni maarufu kwa jina la Mama Africa, alizaliwa katika eneo la Aguata la jimbo la Anambra nchini Nigeria na ndiye mwanzilishi wa kundi la Voice for Senior Citizens of Nigeria.

Amesema, yuko tayari kugombea urais wa Nigeria kutokana na kuwa vijana wa hivi sasa hawaoneshi hamu ya kuchukua madaraka.

Katiba ya Nigeria haina ukomo wa mwisho wa umri wa mtu kugombea urais.

Marekebisho ya sheria ya uchaguzi ya mwaka 2018 yalipunguza miaka ya kuweza kugombea urais kutoka 40 hadi 35 lakini haikuweka ukomo wa umri wa mtu kugombea nafasi hiyo.

Rais wa hivi sasa wa Nigeria Muhammadu Buhari hatoweza kugombea urais mwakani kwani hivi sasa anamalizia kipindi cha pili cha kuwa rais wa nchi hiyo. Bikizee Ezeanyaeche amejiunga na orodha kubwa ya wanasiasa waliojitokeza kugombea kiti hicho huko Nigeria akiwemo mkuu wa chama cha All Progressive Congress (APC), Ahmed Rinubu, Mkuu wa Mkoa wa Ebonyi, David Umahi na Seneta wa Abia Kaskazini, Orji Uzor Kalu.

Hapa chini tumeweka kipande cha video alipotangaza nia yake

(Visited 49 times, 1 visits today)

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

error: Content is protected !!