Nuru ya Uislamu inapoingia haichagui kabila wala rangi, wala ukoo na wala nchi anayotoka mtu. Mbele ya Mwenyezi Mungu wanadamu wote ni wamoja. Wote wameumbwa kwenye nafsi moja. Katika mitandao ya kijamii sasa hivi kumeenea mkanda mmoja wa video unaomuonesha raia mmoja wa Korea Kusini akielelezea jinsi alivyoathiriwa na tartili ya Qur’ani Tukufu ikiwa ni mara yake ya kwanza kusikiliza Qur’ani tangu awe Muislamu.

Katika mkanda huu wa video hapa chini, anaonekana mmoja wa Waislamu wa Korea ambaye ndiyo kwanza amesilimu akielezea jinsi alivyoathirika moyoni na kupata hisia za kipekee wakati aliposikiliza kwa mara ya kwanza tartili ya Qur’ani Tukufu iliyokuwa inasomwa na kijana mdogo raia wa Morocco. Muislamu huyu mpya anaelezea kwa kusisitiza kwamba, moyo wake umepata hisia  za kipekee kabisa kutokana na kwamba sasa ameisikiliza Qur’ani kwa mapenzi makubwa.

Anasema, kabla ya kusilimu aliwahi kusikia Qur’ani ikisomwa, lakini tatrili ya leo ni ya kwanza kabisa kuisikiliza baada ya kusilimu na amehisi kuna tofauti kubwa. Anasema, kabla ya kuwa Muislamu alikuwa akiisikia Qur’ani kwa masikio yake tu, maneno yakiingia sikio hili na kutokea sikio hili. Lakini leo ameisikiliza kwa dhati yake yote.

Baada ya kumaliza kusikiliza tartili hiyo ya Qur’ani alikuwa zimemuondokea zile hisia alizokuwa nazo za kujihisi amepotea kwenye jangwa lenye kiza kwani sasa anaona nuru ya Qur’ani imemwangazia. Anasema, kijana huyo raia wa Morocco amebarikiwa kuwa na sauti nzuri na yeye anatamani siku moja aweze kusoma Qur’ani kama anavyosoma kijana huyo Mmorocco.

(Visited 54 times, 1 visits today)

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

error: Content is protected !!