Rais Vladimir Putin wa Russia ametumia aya za Qur’ani Tukufu katika siku ya umoja na mshikamano nchini humo. Aya hizo ni zile zilizotarjumiwa kwa lugha ya Kirusi. Aya hizo ni ya 23 ya Surat al Shura na 128 ya Surat al Nahl.

Mtandao wa habari wa “msdernet,” umeripoti habari hiyo na kuongeza kuwa, Rais Vladimir Putin amehutubia umma kwa njia ya video katika Siku ya Taifa ya Umoja na Mshikamano, sherehe ambazo zimehudhuriwa na wawakilishi wa dini tofauti za Russia.

Katika hotuba yake hiyo, Rais Putin amesoma tarjama ya aya ya 23 ya Surat al Shura na aya 128 ya Surat al Nahl kwa lugha ya Kirusi na kusema, aya hizo za Qur’ani Tukufu zinazungumzia ihsani, watu kupendana, watu kuishi pamoja kwa wema na malipo bora ya waja wema wanaotekeleza mafundisho ya aya hizo.

Putin alinukuu pia mistari ya vitabu vya dini nyingine kama Biblia na kutilia mkazo raia wote wa Russia kuishi pamoja kwa salama na amani na kila mmoja kuheshimu itikadi za mwenzake.

Katika sehemu moja ya hotuba yake, rais huyo wa Russia amesema, sote tunaona matokeo mabaya ya vitendo vya watu wanaoeneza fitna kupitia kuvunjia heshima matukufu ya kidini na kujeruhi hisia za wafuasi wa dini kwa madai ya uhuru wa kujieleza. Huko nyuma pia, Rais Vladimir Putin wa Russia alimlaumu Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa kwa kuunga mkono kuvunjiwa heshima Mtume Muhammad SAW kwa madai ya uhuru wa kujieleza.

(Visited 39 times, 1 visits today)

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

error: Content is protected !!