Mahakama moja nchini India imewafutia kesi viongozi wote wa zamani na wa hivi sasa wa chama tawala waliohusika katika jinai ya kuvunja msikiti wa kihistoria nchini humo mwaka 1992.

Gazeti la Daily Mail limeripoti habari hiyo na kuongeza kwamba mahakama hiyo ya India imewafutia kesi watuhumiwa 32 wa jinai ya kuushambulia na kuuvunja Msikiti wa kihistoria wa Babri nchini humo mwaka 1992. Jinai hiyo ya wafuasi wa dini ya Kihindu (Kibaniani) ilizusha machafuko makubwa na kupelekea watu 2,000 kuuawa wengi wao wakiwa ni Waislamu.

Uliokuwa Msikiti wa Babri huko Ayodhya India kabla ya kuvunjwa na Mabaniani (Wahindu)

Viongozi wanne wa ngazi za juu cha chama cha kisoshalisti cha Mabaniani kiitwacho Bharatiya Janata Party (BJP) na ambacho ndicho kinachotawala India hivi sasa walikuwa wanakabiliwa na mashtaka ya kutoa hotuba za uchochezi zilizopelekea kuvunjwa msikiti huo. Viongozi hao wamedai kuwa, Wahindu walijichukulia hatua mikononi mwao na kwenda kuuvunja msikiti huo. Wamedai eti wao hawakuhusika.

Hukumu hiyo ilitolewa jana Jumatano, Septemba 30, 2020 ikiwa ni mwaka mmoja baada ya Mahakama Kuu ya India kuunga mkono kujengwa maabadi ya Mabaniani kwenye eneo la Msikiti huo. Wahindu wanadai kwamba eti sehemu ya Msikiti huo huko Ayodhya, ndipo alipozaliwa mmoja wa miungu wao.

Mwaka jana 2019, Mahakama Kuu ya India iliwaunga mkono Wahindu hao ikawaruhusu wajenge maabadi yao katika sehemu ya Msikiti huo na kuwapa Waislamu sehemu nyingine ya kujenga Msikiti.

(Visited 65 times, 1 visits today)

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

error: Content is protected !!