Rais mteule wa Marekani, Joseph Robinette Biden Jr.  maarufu kwa jina la Joe Biden ameanza kufuatilia njia za kuruhusu Waislamu kuingia nchini Marekani na kubatilisha marufuku iliyowekwa na rais wa hivi wa nchi hiyo, Donald Trump. Itakumbukwa kuwa, katika ahadi zake wakati wa kampeni za uchaguzi, Joe Biden aliahidi kuruhusu Waislamu kuingia nchini Marekani kuanzia siku ya kwanza kabisa ya kuingia katika Ikulu ya nchi hiyo, White House.

Gazeti la Washington Post limeripoti kuwa, Biden ameshaanza harakati za kutoa “dikrii” ya utekelezaji ya kuruhusu Waislamu kuingia nchini Marekani, kuanzia siku ile ile atakayoapishwa kuwa Rais wa 46 wa Marekani.

Maandamano ya Waislamu nchini Marekani

Gazeti hilo limezinukuu duru za karibu na Joe Biden zikisema kwamba, rais huyo mteule wa Marekani yuko mbioni kufuta marufuku iliyowekwa na Donald Trump ya kuingia Marekani raia wa nchi zenye Waislamu wengi. Mwaka 2017 Trump alitoa amri ya utekelezaji ya kupiga marufuku raia wa nchi kadhaa za Waislamu wengi, kuingia nchini Marekani, akiwatuhumu kuwa eti ni magaidi. Duru zilizo karibu na Biden zimedokeza pia kwamba rais huyoi mteule wa Marekani anafuatilia pia kuirejesha Marekani katika Mkataba wa Hali ya Hewa wa Paris na kwenye Shirika la Afya Duniani (WHO).

Kabla ya hapo, Baraza la Uhusiano wa Uislamu na Marekani (CAIR) lilikuwa limetoa tamko na kuitaka serikali ijayo ya nchi hiyo kunyanyua kiwango cha haki za kiraia, kuleta usawa baina ya watu wa rangi na vizazi mbalimbali na kufuata siasa za kiuadilifu katika masuala yake ya nje sambamba na kuwashirikisha vilivyo Waislamu katika sekta mbalimbali za utendaji serikalini. Baraza la Uhusiano wa Uislamu na Marekani (CAIR) ndiyo taasisi kubwa zaidi ya kupigania uhuru wa kiraia wa Waislamu nchini humo. Mambo ya kimsingi yanayopiganiwa na chombo hicho ni kulindwa haki za kiraia, kunyanyua welewa wa watu kuhusu Uislamu, kueneza uadilifu na kuwatia nguvu Waislamu nchini Marekani.

(Visited 15 times, 1 visits today)

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

error: Content is protected !!