Ni shairi kutoka kwa Ali Othman Masoud wa Zanzibar

*****

Hivi hii rangi yangu, weupe wa kusifika,

zawadi ya Bwana Mungu, wahadahu Lasharika,

niwadharau wenzangu, huku siko kupotoka?

Si jambo la kujilabu.

*****

Hata kama nina kimo, njonjoti la uhakika,

nidharau mbirikimo, kwa kuifanya dhihaka,

niwatiye kwenye shimo, daima wasijetoka,

Si jambo la kujilabu.

*****

Sababu ya hizi nguvu, nibene ninachotaka,

mnene kwa zangu mbavu, chochote chakamatika,

Niwaone wapumbavu, dhaifu waliochoka?

Si jambo la kujilabu.

*****

Au kwa wangu usomi, digirii nazishika,

hajifanya ndio mimi, msomi wa kusifika,

hawapiga wao ngumi, skuli wasiofika,

Si jambo la kujilabu.

*****

Miye hasa nina mali, majumba yalojengeka,

magari kila mahali, tena yanoendesheka,

watu wenye idhilali, hainama hawacheka,

Si jambo la kujilabu.

*****

Itazame   yangu sura, muili uloumbika,

wenzangu naona vyura, wao si wa kutajika,

miye kwao ndio bora, sababu natizamika,

Si jambo la kujilabu.

******

Ni kipi cha kujilabu, maisha yaso hakika,

Mungu anazo adabu, ambazo ameziweka,

kwetu akiziratibu, waja tutamalizika,

Na tena akajilabu.

****

Ali Ben Othman, Zanzibar 29/9/2020

(Visited 27 times, 1 visits today)
One thought on “Ni kipi cha kujilabu?”

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

error: Content is protected !!