Hatimaye Baraza la Wawakilishi la Marekani limepasisha muswada wa kupambana na chuki dhidi ya Uislamu licha ya kupingwa na wabunge wote wa chama cha Republican cha Donald Trump, raislamu wa zamani wa Marekani mwenye chuki na uadui mkubwa na Uislamu na Waislamu.

Baraza la Wawakilishi la Marekani limepasisha muswada huo kwa kura 219 za ndio mbele ya 212 za hapana. Muswada huo uliwasilishwa bungeni hapo na Ilhan Omar, Mbunge Muislamu mwenye asili ya Somalia.

Kwa mujibu wa muswada huo, sasa kutafunguliwa ofisi maalumu ndani ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani ambayo itakuwa na jukumu la kupambana na chuki dhidi ya Uislamu.

Ikumbukwe kuwa hakuna mbunge hata mmoja wa chama cha Republican aliyeupigia kura ya ndio muswada huo.

Vitendo vya chuki na uadui vimeenea sana nchini Marekani na vinafanywa waziwazi na hata na wanasiasa nchini humo. Kutokana na kuongezeka chuki hizo, Mbunge Ilhan Omar wa chama cha Democratic ameamua kuwasilisha muswada bungeni wa kuweka vizingiti vya kuzuia siasa za chuki na uadui dhidi ya Waislamu. Katika muswada huo, Ilhan Omar amependekeza kuundwe kitengo maalumu ndani ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani ambacho kitapambana na siasa za chuki na uadui zinazofanywa na maadui wa Uislamu.

Vile vile mbunge huyo Muislamu amependekeza kuwa, kitengo hicho cha Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani kiwe kinatoa ripoti yake kila mwaka kuhusu vitendo vya chuki, unyanyasaji na udhalilishaji wanaofanyiwa Waislamu.

Ilhan Omar, Mbunge aliyepigania na kufanikiwa kupasisha muswada wa kupambana na chuki dhidi ya Uislamu nchini Marekani

Muswada huo umepasishwa wiki chache baada ya mbunge wa chama cha Republican, Lauren Boebert kutumia mitandao ya kijamii kumdhalilisha Mbunge Ilhan Omar kutokana na kuwa kwake Muislamu na alitumia kisingizio cha uhuru wa kusema kutoa matusi dhidi ya Uislamu na kuihusisha dini hiyo takatifu na vitendo vya kigaidi.

Ikumbukwe pia kuwa vitendo vya chuki na uadui dhidi ya Uislamu na Waislamu vilipamba moto zaidi katika kipindi cha miaka minne ya urais wa Donald Trump huko Marekani.

Wakati wa kampeni za uchaguzi, rais wa hivi sasa wa Marekani, Joe Biden aliahidi kupambana na ubaguzi na chuki dhidi ya Waislamu lakini hadi hivi sasa ameshindwa kufanya chochote cha maana.

(Visited 37 times, 1 visits today)

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

error: Content is protected !!