Mahakama Kuu nchini Misri imepasisha hukumu ya kutolewa adhabu kwa yeyote atakayechapisha Msahafu na Hadithi za Mtume kiholela na bila ya kibali.

Mtandao wa habari wa al Misr al Yaum umeripoti habari hiyo na kuongeza kuwa, hukumu iliyotolewa na Mahakama ya Jinai ya Cairo kuhusu kuwa na nguvu za kisheria kipengee cha 5 cha kifungu cha 2 cha sheria ya miaka 102 kilichoongezwa mwaka 1985, imepasishwa na Mahakama Kuu ya Misri.

Sheria hiyo inahusiana na kuchapisha Msahafu na Hadithi za Mtume bila ya kibali na imesema wazi kwamba yeyote atakayechapisha Msahafu na Hadithi za Mtume bila ya kibali ni muhalifu na anastahiki kufunguliwa mashtaka na kupewa adhabu. Kibali cha kuchapisha Msahafu na Hadithi za Mtume, kinatolewa na Baraza la Utafiti wa Kiislamu la Cairo kwa ajili ya nchi nzima ya Misri.

Mahakama Kuu ya Misri imesema, hukumu hiyo mpya imetolewa ili kudhamini usalama wa Misahafu inayochapishwa nchini humo. Imesema, kuna maadui wa Uislamu bali hata baadhi ya makundi ya kigaidi, yanachapisha Misahafu kwa kupotosha maana ya aya za Qur’ani na Hadithi za Mtume ili kuhalalisha vitendo vyao vya kigaidi. Hivyo yeyote anayefanya hivyo, anahesabiwa ni mhalifu anayestahiki kupewa adhabu kisheria.

Ni vyema kusema hapa kwamba, viwanda vya kupiga chapa nchini Misri, vinachapisha Qur’ani kwa riwaya mbalimbali za usomaji. Hata hivyo riwaya kuu ni ya Warsh ambayo ndiyo inayotumika sana katika nchi 5 za eneo la Sahel za kaskazini magharibi mwa Afrika. Nchi hizo ni Burkina Faso, Chad, Mali, Mauritania na Niger. Kabla ya Msahafu kumfikia msomaji, hupitia hatua 5 za kuangaliwa na kuhaririwa maandishi yake ili kusiwe na kosa hata dogo mno la uchapishaji.

(Visited 81 times, 1 visits today)

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

error: Content is protected !!